KASHFA
ya ukahaba iliyokuwa inakikabili Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) pamoja na
maandamano na migomo, vimekuwa vikimnyima usingizi Makamu Mkuu wa chuo
hicho, Profesa Idris Kikula.Profesa Kikula alibainisha hayo mwishoni mwa wiki wakati akizungumza na walimu pamoja na wanafunzi wa chuo hicho kwenye hafla ya kukabidhi makombe pamoja na medali walizoshinda kwenye mashindano ya SHIMMUTA na TUSA.
Alisema kashfa hiyo ilimnyima usingizi kiasi kwamba ilifika mahali akajiuliza anafanya nini katika chuo hicho, ndipo alipoamua kufanya uchunguzi wake binafsi.
“Kwa kweli ile kashfa ya ukahaba wa wanafunzi iliyokuwa inasemwa hapa chuoni ilikuwa inaninyima usingizi… ilifika wakati nikajiuliza sasa nafanya nini hapa?” alisema Profesa Kikula.
Profesa Kikula alisema aliamua kufanya uchunguzi ili kujua kama habari zinazotangazwa kwenye mitandao ya kijamii kuhusiana na chuo hicho ni za kweli, lakini alibaini zilikuwa ni njama za baadhi ya watu waliotaka kukichafua chuo kwa maslahi binafsi.
Alisema katika uchunguzi wake alibaini kuwa kuna baadhi ya wasichana wanaojiuza mjini hapa ambao walikuwa wanajiita wanafunzi wa UDOM wakati si kweli.
Mbali ya kashfa hiyo ya ukahaba, mambo mengine yaliyokuwa yanamnyima usingizi kuwa ni pamoja na maandamano, migomo na migogoro iliyokuwa ikiendelea chuoni hapo.
“Miaka mitatu iliyopita UDOM ilichafuka kiasi kwamba wanafunzi waliokuwa wanahitimu walishindwa kuajiriwa mahali popote kwa sababu walionekana wakorofi na wasiokuwa na maadili,” alisema.
Hata hivyo, alisema hivi sasa hali imetulia na wanafunzi wanaotoka chuoni hapo wamekipa sifa nzuri chuo hicho kwa uhodari wao kazini.
-Tanzania Daima

No comments:
Post a Comment