CHAZ BABA UKIENDEKEZA KUMPIGA MKEO, JELA INAKUHUSU

Charles Gabriel ‘Chaz Baba’.
KWAKO jembe, Charles Gabriel ‘Chaz Baba’. Mwalimu wao kwenye muziki wa dansi Bongo. Uwezo wako nautambua, nimekuwa shabiki wako kwa muda mrefu kidogo.Ni matumaini yangu uko poa, unaendelea na mishe zako kama kawaida.
Mimi mzima, namshukuru Mungu maisha yanasonga. Jukumu langu la kuandika na kukosoa linaendelea na leo nimekukumbuka wewe.Dhumuni la kukumbuka leo kwanza ni kukukemea kwamba suala la kuthubutu kushika kitu kizito, kunyanyua mkono na kumtwanga mtu si jambo jema, halifai kuigwa hata kidogo.
Ndugu yangu, hivi kwanza unafikiria nini ukichukua kitu kizito na kumpiga nacho mwenzako?Mbona zipo njia nyingi za kufikisha ujumbe wako kwa mtu na akajua umekasirika, lakini si kumtwanga na kitu kizito au chenye ncha kali ambacho unajua fika kwamba utamsababishia maumivu makali mwilini.
Kwa kitendo ulichokifanya kwa mkeo hivi karibuni hakikuwa cha kiungwana. Ulimtwanga kiasi ambacho kwa macho ya kawaida tu, inaonesha aliumia sana.Sitaki kujua alikuudhi nini, lakini ustahimilivu unatakiwa katika maisha ya kila siku.
Hata iweje yule ni mkeo. Unajisikiaje kumuona akiwa na majeraha chungu nzima mwilini ambayo umesababisha wewe? Si sawa kabisa!Wewe ni kioo cha jamii, unategemea jamii itajifunza nini kupitia tukio kama lile ulilolifanya? Unavyotakiwa kujichunga wewe ni mara mia zaidi ya vile anavyojichunga mwenzangu na mimi kule Tandale Kwa Mtogole.
Jamii inawatazama mastaa kama kioo chao, wanaamini kwamba nyinyi ni watu wema. Wanaamini mnajua kujitoa, mna upendo na mna nguvu ya kukemea maovu kwenye jamii na watu wakabadilika.
Umeshindwa kustahimili hasira zako, ona sasa jamii nzima ilijua kwamba umemdunda mkeo kiasi cha kuwafanya hata wale mashabiki wanaokufuatilia waone kuwa hukumtendea haki mkeo.Kumpiga mtu siyo dawa ya kutibu tabia au tatizo lake.
Unaweza ukampa mtu adhabu nyingine ambayo kwa macho ya kawaida inaweza kuonekana ndogo lakini kumbe ni nzito na ikamfanya mtu aone aibu kwa kipindi kirefu kama si maisha yake yote.Kunyanyua mkono na kumpiga mtu ni tabia.
Ukiiendekeza unaweza kufika pabaya ambapo pengine hata hujawahi kutegemea kama ipo siku unaweza kufika. Hatupendi itokee lakini sheria zipo.Utakuja siku ujibiwe vibaya na mtu sehemu, ukachukua silaha na kumdunda kama ulivyofanya kwa mkeo, sheria ikachukua mkondo wake, jela itakuwa inakuhusu.Achana na desturi ya kupiga, tumia njia mbadala kumuadhibu mtu.
Kupiga hakusaidii. Kwa leo acha niishie hapo lakini ni matumaini yangu utabadilika na kuwa mtu safi kama macho ya wengi yanavyokuangalia. Ni hayo tu!

No comments:

Post a Comment

 
Support : WELCOME AGAIN MDADISI
Copyright © 2011. MDADISI WA MAMBO
THIS IS MDADISI
Proudly powered by Blogger